JINSI ISIVYOWEZEKANA MTU KUOKOKA BILA MAOMBI
Jumapili 20. 2. 2000 itakuwa ni siku ya uzinduzi wa
Operesheni Maliza Kazi (YOHANA 4:34; 17:4 ). Siku ya kunyakuliwa kwa Kanisa
inazidi kukaribia. Bado kitambo kidogo sana, Yesu ajaye, anakuja wala
hatakawia, (WAEBRANIA 10:37), hivyo huu ni wakati wa kumaliza kazi tuliyopewa
ya kuwaleta watu kwa Yesu; kwa kishindo zaidi kuliko tulivyoanza. Siku hiyo ya
jumapili 20.2. 2000, tunatazamia kuwaona watu wageni maelfu-elfu ambao
hawawezi kutosha katika mfumo wa ibada
wa sasa, na hivyo kuanzia siku hiyo tutaongeza ibada nyingine. Sasa basi, ni
makusudi ya somo letu la leo, kujifunza yatupasayo kufahamu ili tupate kuona
maelfu-elfu wakija na kuokoka siku hiyo. Tunajifunza somo hili kwa kulitafakari
katika vipengele vinne vifuatavyo:-
( 1 ). JINSI MTU ASIYEOKOKA ALIVYO KATIKA ULIMWENGU WA ROHO
( 2 ). JINSI ISIVYOWEZEKANA MTU KUOKOKA BILA MAOMBI
( 3 ). JINSI YA KUFANYA MAOMBI KIVITENDO
( 4 ). MAMBO YA KUZINGATIA
( 1 ). JINSI MTU ASIYEOKOKA ALIVYO KATIKA ULIMWENGU WA ROHO
Watu wote tuliokolewa, tuko katika ufalme wa Mungu. Bwana
Yesu ndiye Mtawala wetu. Upande wa pili, kwa jinsi hiyohiyo, watu wote ambao
hawajaokoka, wako katika ufalme wa Ibilisi. Shetani ndiye mtawala wao.katika
ufalme wa Shetani, watu hawa ni watumwa wa Ibilisi, ni mali yake Ibilisi, ni
watoto wa Ibilisi ( 1 YOHANA 3:8-10; YOHANA 8:34 ). Watu hawa walioko katika
ufalme wa Shetani, pia ni wafungwa katika gereza la Shetani, na Shetani hataki
kuwaachia. Ni mpaka apatikane mwenye nguvu zaidi, wa kuwafungua ( LUKA 4:18 )
Wafungwa hawa wanalindwa vikali na Shetani ili kuhakikisha hawatoki katika
nyumba yake, na anawaita VITU VYAKE, na
mateka wake ( LUKA 11:21-22 ).Siyo hilo tu. Akili zao zimetiwa giza,
wamepofushwa fikra zao na kujazwa kila namna ya ujinga ili isiwazukie nuru ya
Injili ya wokovu ( WAEFESO 4:17-19;2WAKORINTHO 4:3-4 ).Wamedanganywa na Ibilisi
baba wa uongo. Kwa kila namna ya uongo, na kufanya wachukie kweli ya wokovu, na
kuona kwamba hakuna kuokoka duniani, dini zao zinatosha n.k. ( UFUNUO 12:9; YOHANA 8:43-45 ).
Kujaribu kuwaarika watu wa jinsi hii kuja kusikia Injili au kujaribu
kuwashuhudia katika hali hii, ni kupoteza muda wetu. Kwanza kabisa Shetani
hawezi kuwaachia watoke katika ufalme wake na pia kwa jinsi walivyodanganywa na
kupofushwa fikra zao. Hakuna lolote la wokovu linaloweza kueleweka kwao.
( 2 ). JINSI ISIVYOWEZEKANA MTU KUOKOKA BILA MAOMBI
Kama tulivyotangulia kuona, Shetani hawezi kutuachia
tuvichukue VITU VYAKE kiulaini, na kuviweka katika ufalme wa Mungu ni mpaka
tupambane naye, tupigane naye vita na kumshinda, kisha kumnyang’anya mateka
wake bila yeye kupenda kwa sababu tu amezidiwa nguvu. Kwa namna ile ile ambayo
Farao hakuweza kuwaachia Waisraeli kiulaini, mpaka pale aliposhindwa. Vivyo
hivyo hawezi kuviachia “vitu vyake” mpaka tupambane naye kwanza na kumshinda,
na kumlazimisha kumuachia. Vita hii inaitwa VITA YA KIROHO (spiritual warfare)= ( WAEFESO 6:11-12; 2WAKORINTHO 10:3-4
).Siraha kubwa ya kivita tunayopaswa kutumia ni MAOMBI. Katika WAEFESO 6:11-20,
tunaona siraha zote za vita hizi zikitajwa. Hapa tunaona siraha saba
zinazotumika katika vita vya kiroho, zikitajwa. Hata hivyo, siraha ya mwisho,
siraha ya saba , maombi, inapewa uzito mkubwa kuliko zote zilizotangulia.
Siraha sita za mwanzo zinatajwa zote katika mistari mine ( MST 14-17 ), lakini
mistari yote mitatu (MST 18-20 ), inazungumzia
silaha moja ya maombi, kuonyesha uzito wake ikilinganishwa na zile
nyingine. Maombi, ndiyo ufunguo wa kumshinda Shetani na kumnyanganya vitu
vyake. Kwa maombi, kwa jina la Yesu, tunamfunga Shetani na majeshi yake, na
kuhakikisha hawafurukuti na kumnyang’anya silaha zake anazozitegemea, kisha
tunawachukua mateka wake na kuwaongoza katika ufalme wa Mungu ( MATHAYO
16:18-19; LUKA 11:21-22 ). Tunapokwenda kumshuhudia mtu juu ya wokovu au
kumwalika aje kusikia Injili, bila kwanza kumtoa kifungoni, baada ya kumzidi
nguvu Mfalme wake Ibilisi, kufanya hivyo ni kazi bure. Ni vigumu sana kupata
matokeo yanayotarajiwa. Kwa ufupi, kabla ya kufanya maombi tusijaribu kwenda
kushuhudia au kuwaalika watu kusikia
Injili. Matokeo yake yatakuwa hafifu. Hata kama wataisikia Injili, wataisikia
wakiwa katika hali ya uzezeta, na hawawezi kuokoka.
( 3 ). JINSI YA KUFANYA MAOMBI KIVITENDO
1. Sehemu kubwa
ya maombi yetu, iwe ni maombi ya vita dhidi ya Shetani. Kuharibu ufalme wa
Shetani juu ya mtu anayehusika, kukatilia mbali vifungo vyake juu ya mtu
husika, kama vifungo vya kidini n.k, kusambaratisha uongo wake, ujinga wake,
ganzi na kila namna ya upofu wa fikra au uzezeta aliouweka Shetani ndani ya mtu huyo. Kuharibu
kila kamba za utumwa wa dhambi, iwe ni ulevi, uasherati, uzinzi na kila aina ya
dhambi hizo. Kuamuru mtu huyo husika kutoka katika gereza la Ibilisi na kuwekwa
huru kwa jina la Yesu Kristo ( YOHANA 8:36 )Maombi haya ya mapambano au vita
yachukue theluthi mbili ya muda wetu wa jumla wa maombi. Kama muda wetu wa
maombi ni saa moja basi muda wa maombi
ya vita uwe dakika 40. Kama muda wetu wa jumla wa maombi ni saa tatu basi saa
mbili iwe ni maombi ya kupambana na
Ibilisi.
2. Theluthi moja
ya muda uliosalia wa maombi, tumwombe Mungu sasa amvute mtu huyo aliyewekwa
huru kutoka katika ufalme wa Shetani na kumwingiza katika ufalme wa Mungu.
Abadilishe maisha yake kwa Neno na kumfanya akue katika neno lake bila
kurejezwa tena katika dhambi ( YOHANA 8:44; 10;28-29; 1PETRO 1:23 ).Kama muda
wote wa maombi ni saa moja, dakika 20 zitumike kwa maombi hayo. Kama muda wote
wa maombi ni saa tatu, saa moja itumike kwa maombi haya. Wakati wote maombi
haya yatanguliwe na maombi ya mapambano.
3. Kutajwa kwa
majina ya watu tunaotaka wawekwe huru na waokolewe ni muhimu sana. Maombi
specific au maalum kwa mtu maalum, yanakuwa na nguvu ya ziada. Yeyote
atakayeuambia mlima huu ng’oka ( MARKO 11:23 ). Akauambia mti (mtini) mtu asile
matunda kwako ( MARKO 11:12-14, 20-21). Hauna budi kumwombea mtu maalum kwa
kutaja jina lake maalum ili baadaye tujue matokeo ya maombi yetu, kwa jinsi ile
ile ambavyo wanafunzi wa Yesu walivyoufuatilia ule mtini uliolaaniwa na kujua
matokeo ya maombi yale. “Simon, Simon………nimekuombea wewe” ( LUKA 22:31-32 ).
Katika wanafunzi kumi na wawili, Yesu alichagua mmoja maalum wa kumwombea kwa
jina, ili kuongeza nguvu ya maombi. “Lazaro, njoohuku nje” ( YOHANA 11:43 ), ni
fundisho jingine kwetu. Tutaje majina ya wale tunaotaka watoke nje ya gereza la
Shetani.
( 4 ). MAMBO YA KUZINGATIA.
Imani ni silaha mojawapo pia ya vita vyetu. Tusiangalie
ugumu wa wale ambao hawajaokoka. Tusiangalie nguvu na uwezo wa Shetani, basi
tuangalie nguvu na uwezo wa Yesu aliyemwokoa Sauli na kumfanya Mtume Paulo.
Shetani anaitwa “Mtu mwenye nguvu” bali Yesu anaitwa “Mtu mwenye nguvu kuliko
yeye” ( LUKA 11:21-22 ). Vile vile tuwaombee wale tunaofahamu wanakokaa ili
mwishoni mwa maombi haya tuwaalike kuja
siku ya jumapili tarehe 20.2.2000. Kwa sasa tusiwaalike kamwe. Maombi kwanza,
kualika baaadaye.
No comments:
Post a Comment