HAKIKA ALIKUWA MWANA WA MUNGU
Leo, tunaendelea
kujifunza Sura ya 27 ya Kitabu cha MATHAYO, na tutaangalia MATHAYO 27:
50-66. Katika mistari hii, tunajifunza
juu ya kufa na kuzikwa kwa Yesu.
Tutayagawa mafundisho tunayoyapata katika mistari hii katika vipengele
vitano:-
(1) KUPAZA SAUTI KWA
YESU NA KUITOA ROHO YAKE (MST 50)
(2) HAKIKA ALIKUWA
MWANA WA MUNGU (MST 51-54)
(3) WANAWAKE
KUMTUMIKIA (MST 55-56)
(4) KUZIKWA KWA
YESU (MST 57-61)
(5) KULINDWA KWA
KABURI (MST 62-66)
(1) KUPAZA SAUTI
KWA YESU NA KUITOA ROHO YAKE (MST 50)
Kulikuwa na giza juu ya nchi yote tangu saa sita hadi saa tisa
mchana (MST 45). Baada ya saa tisa
mchana, yaani kati ya saa 9 -10 mchana, ndipo Yesu alipokata roho. Kulikuwa na maana kamili juu ya kila jambo
lililofanyika msalabani. Saa tisa,
ilikuwa ni saa ya kusali ya Wayahudi (MATENDO 3:1). Saa nyingine za sala ilikuwa saa 3 asubuhi na
saa 6 mchana. Saa ya kusali saa 9, ndipo
ulipokuwa wakati wa kutoa DHABIHU YA JIONI (DANIELI 9:21, 1 WAFALME 18:29,
36). Saa hii ya jioni, ndipo Yesu
alipokufa msalabani, na kutolewa kama DHABIHU YA JIONI kwa ajili yetu. Wakati huu pia, ni ambapo mwanakondoo wa
Pasaka alipochinjwa. Yesu Kristo,
alitolewa na kuchinjwa msalabani kama Pasaka wetu, mwanakondoo asiyekuwa na ila
wala waa (1 WAKORINTHO 5:7; 1 PETRO 1:19).
Wakati wa kufa kwake Yesu, ALIPAZA SAUTI YAKE kudhihirisha nguvu
alizokuwa nazo mpaka wakati wa kufa.
Hakika alijitoa MWENYEWE kufa kwa ajili yetu. Kwa kawaida, watu wengi wanapokuwa wanakufa
hawana nguvu ya kupaza sauti namna hii hasa baada ya mateso makubwa namna hii.
Lakini, siyo hilo tu, alipaza sauti yake kwa nguvu, kama TARUMBETA
zilizokuwa zikipigwa wakati wa kutoa dhabihu (HESABU 10:9-10). Hakika, Kristo alikuwa dhabihu kwa Mungu,
hatuna haja tena ya wanyama (WAEBRANIA 10:1-12; WAEFESO 5:2).
(2) HAKIKA
ALIKUWA MWANA WA MUNGU (MST 51-54)
Baada tu ya Yesu kuitoa roho yake, matukio kadha ya miujiza
yalitokea, yaliyowafanya askari waliokuwa wanamlinda kusema “HAKIKA HUYU
ALIKUWA MWANA WA MUNGU”. Sasa, ebu
tuyaangalie matukio haya na maana yake:-
PAZIA LA HEKALU
LIKAPASUKA VIPANDE VIWILI – Ni muhimu kukumbuka kwamba, ulikuwa wakati wa
kusali na kutoa dhabihu ya jioni, katika hekalu. Katika hekalu kulikuwa na Pazia la Hekalu,
lenye urefu wa futi 60 kutoka darini hadi sakafuni. Pazia hili liligawanya kati ya Patakatifu, na
Patakatifu pa patakatifu, au mahali patakatifu sana (WAEBRANIA 9:1-3; KUTOKA
26:33). Ilikuwa hakuna ruhusa ya mtu
yeyote wa kawaida kuingia mahali patakatifu hata kuchungulia kwa dakika
moja. Akifanya hivyo, hukumu yake ni
kifo (HESABU 4:17-20). Mahali patakatifu
waliingia makuhani peke yao. Patakatifu
pa patakatifu, aliingia Kuhani Mkuu peke yake, tena MARA MOJA KWA MWAKA akiwa
na damu aliyoitoa kwa ajili ya nafsi yake na kwa dhambi za watu wengine
(WAEBRANIA 9:6-7). Vilevile kulikuwa na
pazia lililowatenganisha Wayahudi na wale wasio Wayahudi (Mataifa) katika
hekalu. Sasa kwenye saa hii ya kusali
nguvu ya ajabu isiyoonekana iliyararua mapazia na kuyafanya vipande Kila mmoja
akashikwa butwaa pamoja na makuhani.
Pale msalabani, kwa damu yake Yesu, alitupa kila mmoja wetu uwezo wa
kuzungumza na Mungu moja kwa moja bila kupitia kwa Kuhani, na pia alitoa pazia
lililotutenganisha Mataifa na Wayahudi (WAEBRANIA 10:19-20; WAEFESO 2:14-18).
NCHI
IKATETEMEKA – Tetemeko hili liliwafanya
wenye dhambi wote, pamoja na askari waliomlinda kutetemeka kwa hofu. Dhambi huleta hofu kubwa. Siyo hilo tu, nchi ilitetemeka kwa hofu na
woga wa kufunua kinywa chake kummeza Yesu Kristo ambaye damu yake inanena mema
kuliko ya Habili (WAEBRANIA 12:24).
Ikiwa nchi ililaaniwa kwa kumeza damu ya Habili, ni zaidi sana kwa
Yesu. Ilikuwa ni rahisi kufunua kinywa
chake na kuwameza Kora, Dathani na Abiramu na watu wa nyumba zao, waliokuwa
wamemwasi Mungu (HESABU 16:27-34), kuliko kummeza Yesu asiyekuwa na doa. Hivyo nchi ilitetemeka. Vilevile nchi ilitetemeka kwa ajili ya watu
wenye dhambi waikaao (AMOSI 8:4-8).
MIAMBA
IKAPASUKA – Wanadamu wakimpuuza Mungu na
kuacha kumsifu Yesu mawe yatapiga kelele.
Hapa yalifanya hivyo. Siyo hilo
tu, hapa Yesu Kristo aliyaendea majeshi ya Shetani kwa ghadhabu na hasira kuu
kwenda kuyavua mamlaka. Hasira na
ghadhabu hiyo ilifanya miamba kupasuka na nchi kutetemeka (NAHUMU 1:6; WAAMUZI
5:4; ZABURI 68:7-8). Vilevile Yesu Kristo
ni mwamba, miamba yote hupasuka mbele zake.
Siyo hilo tu kwa imani katika damu ya Yesu, mioyo yetu iliyo migumu kama
jiwe au miamba hupasuliwa na kufanywa mioyo laini kama ya nyama (EZEKIELI
36:26-27). Ndipo tunapoweza kuziona amri
zake ni rahisi mno maana tumetakaswa, tumetahiriwa mioyo yetu.
MAKABURI
YAKAFUNUKA – Makaburi ya Watakatifu
waliojulikana Yerusalemu, yalifunuka wakati wa kufa kwa Yesu na kuleta utisho
mkuu. Hata hivyo, walitoka makaburini
mwao BAADA YA KUFUFUKA KWAKE YESU kwa kuwa Yesu ndiye mzaliwa wa kwanza wa
waliokufa, limbuko lao waliolala (1 WAKORINTHO 15:20; UFUNUO 1:5). Baada ya Yesu kufufuka, watakatifu hawa
walifufuka nao na kuwatokea wengi Yerusalemu, Tukimwamini Yesu, kama
alivyokwenda mbinguni, sisi nasi tutakwenda huko. Kama alivyofufuka, sisi nasi tutafufuliwa
katika Ufufuo wa Uzima (YOHANA 5:28-29).
Akida, yaani mkuu wa kikosi, na maaskari wenzake walipoyaona haya, NDIPO
wakaogopa sana, wakisema, Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu. Haupaswi kungojea kuyaona haya, ndipo tumkiri
Yesu kuwa ni Mwana wa Mungu, au ni Bwana na Mwokozi wa Ulimwengu. Hatupaswi kungojea haya ndipo tukubali
wokovu. Tutakuwa tumechelewa. Wakati wa Kunyakuliwa kwa Kanisa
kutakakofanyika wakati wowote kuanzia sasa, Watakatifu watatoka makaburini
namna hii na wenye dhambi wataogopa na kutetemeka, na kumkiri Yesu wakati wamechelewa. Watakaochukuliwa ni wale waliookoka pasipo
kuona, bali kwa imani (2 WAKORINTHO 5:7).
(3) WANAWAKE
KUMTUMIKIA MUNGU (MST 55-56)
Ni uongo wa Shetani kwamba wanawake hawawezi kuwa Watumishi
wa Mungu, wakahubiri, wakafundisha, wakatoa pepo au kumtumikia Mungu kwa namna
nyinginezo. Wanawake kumtumikia Mungu,
ni jambo la Ki-Biblia hasa. Nyakati hizi
za mwisho, Roho wa Mungu atamwagwa kwa WOTE, binti watatabiri (kuhubiri ni
kutabiri pia) na Roho huyu wa Mungu atamwagwa kwa WATUMISHI WA MUNGU WANAUME NA
WANAWAKE (MATENDO 2:17-18). Nyakati za
Kanisa la Kwanza, wanaume na wanawake, wote walikuwa watendakazi, wakilihubiri
Neno na kulifundisha (MATENDO 8: 1, 4).
Inatupasa kufuata mfumo huu wa ki-Biblia. Mara kwa mara, katika Biblia, wanawake, wamekuwa
na ujasiri wa kumtumikia Mungu na kuwa wanyenyekevu na watii kwa Yesu Kristo na
Neno lake, kuliko wanaume. Hapa tunaona
wanawake waliomfuata Yesu kutoka Galilaya, karibu maili 100 kutoka Yerusalemu,
wakija kumtumikia Yesu. Hapa msalabani,
hawakuwako wanafunzi wale kumi na moja wa Yesu kasoro Yohana (YOHANA 19:
25-26). Wengi walikuwa wanawake
waliokuwa wakijipiga vifua na kumwombolezea (LUKA 23:27). Wanawake walikuwepo msalabani mpaka mwisho na
tena walikuwapo kwenye mazishi yake (MST 61) na pia wanawake ndiyo waliokuwa wa
kwanza kwenda kulitazama kaburi siku ya kufufuka kwa Yesu (MATHAYO 28:1). Mwanamke ndiye aliyewapelekea habari za
kufufuka kwa Yesu, Petro na Yohana, na kuwatia moyo, NDIPO nao wakachangamka! Hapo mwanzo, walikuwa wamekata tamaa na
kwenda kuvua samaki (YOHANA 20:1-3; 21:1-3).
Mwanamke Priska au Prisila alikuwa tayari kukatwa kichwa kwa ajili ya
Injili aliyokuwa anaihubiri Paulo na Mwanamke Fibi aliwasaidia wengi mno
(WARUMI 16:1-3). Shime wanawake, tutende
kazi ya Bwana! Wanaume pia tupate changamoto kwa watendakazi wanawake ambao
wanatenda kazi ya Mungu kwa bidii pamoja na majukumu mengi ya kifamilia waliyo
nayo.
(4) KUZIKWA KWA
YESU (MST 57-61)
Baada ya kufa, Yesu
alizikwa. Sisi nasi baada ya kufa pamoja
naye inatupasa kuzikwa pamoja naye kwa njia ya Ubatizo (WAKOLOSAI 2:12). Ikiwa tumeifia dhambi kwa kufa pamoja na
Kristo kweli, hatuwezi kuwa wabishi kuhusu ubatizo wa maji tele baada ya
kuokoka. MAITI HASEMI, HUZIKWA TU! Tena kumzika maiti, ni kumfunika kabisa kwa
udongo, siyo kumnyunyizia udongo usoni.
Vivyo hivyo, ubatizo ni wa maji tele (YOHANA 3:22-23). Mwanafunzi wa Yesu aliyekubaliwa kupewa
maiti, alikuwa mtu tajiri, mstahiki (Mheshimiwa), mtu wa baraza ya mashauri
(MATHAYO 27:57-58; MARKO 15:42-43). Watu
tuliookoka tulio matajiri, wenye vyeo, wenye elimu, inatupasa tuyatumie hayo
kwa ajili ya kuishindania Injili.
(5) KULINDA KWA
KABURI (MST 62-66)
Wakuu wa Makuhani
walimwita Pilato, BWANA, lakini Yesu walimwita MJANJA (MST 62-63). Ndivyo walivyo viongozi wengi wa dini
leo. Walililinda kaburi na kulitia
muhuri au lakiri ambayo siyo rahisi kuifungua, bila kujulikana, wakafikiri ni
salama, lakini Yesu akafufuka. Hata
tukiwazuia watu kuifuata kweli kwa kuwazuia kwa lakiri, wataifuata kweli tu. Neno la Mungu halifungwi (2 TIMOTHEO 2:9).
FULL GOSPEL
No comments:
Post a Comment