HATARI YA KUIPENDA NAFSI
Tunaendelea tena leo, kujifunza Kitabu cha YOHANA katika
Biblia zetu. Leo, tunatafakari kwa
makini YOHANA 12:12-28. Katika mistari
hii, tutajifunza “HATARI YA KUIPENDA NAFSI“, pamoja na mengine mengi. Tutayagawa mafundisho tunayoyapata katika
mistari hii, katika vipengele tisa:-
(1) KUINGIA KWA YESU YERUSALEMU (MST. 12-15);
(2) UWEZEKANO WA WANAFUNZI WA YESU KUSHINDWA KUYAFAHAMU
MAMBO FULANI MWANZONI
(MST. 16);
(3) SABABU YA MKUTANO MKUBWA KUMLAKI YESU (MST. 17-18);
(4) KUSHINDWA KWA SHETANI KUZUIA MAFANIKIO YA INJILI (MST.
19);
(5) UTARATIBU WA KUMWONA YESU (MST. 20-23);
(6) JINSI YA KUTOA MAZAO MENGI (MST. 24);
(7) HATARI YA KUIPENDA NAFSI (MST. 25);
(8) MASHARTI NA FAIDA ZA KUMTUMIKIA MUNGU (MST. 26);
(9) JINSI YA KULIONA JINA LA BWANA LIKITUKUZWA KWETU (MST.
27-28).
(1) KUINGIA
KWA YESU YERUSALEMU (MST. 12-15)
Wakati huu, ilikuwa siku nne kabla ya Sikukuu ya
Pasaka. Watu wengi walitoka mbali sana
na kuja kwenye Sikukuu alizoziamuru Bwana, ili kuja kumwabudu. Nyakati za Biblia, Mungu hakupendezwa hata
kidogo kumwona mtu yeyote anabaki nyumbani wakati anapotakiwa kwenda katika
ibada. Mungu aliweka adhabu kali kwa
yeyote aliyepuuza kuhudhuria ibada.
Adhabu hii, iliambatana na kukosekana kwa mvua na kupigwa kwa auni; na
ilienea katika jamii yote, au taifa lote ikiwa walipuuza kuhudhuria ibada
(ZEKARIA 14:17-19). Ili kukwepa adhabu
hii, watu walitoka mbali sana kwa wingi wao, na kuja kuhudhuria Ibada. Hata leo, ni vivyo hivyo. Mungu hapendezwi na yeyote anayepuuza
kuhudhuria ibada zote. Tunajikosesha
baraka tele na kujiletea maafa, ikiwa hatuhudhurii ibada zote. Watu hawa waliposikia Yesu anakuja Yerusalemu
walitoka nje kwenda kumlaki. Habari za
kuja kwa yesu kulinyakua Kanisa, tayari zimekwisha kutufikia (UFUNUO 22:7;
3:11; WAEBRANIA 10:37). Ni muhimu kwa
kila mmoja wetu kujiuliza kama tumejiweka tayari kumlaki Yesu na kuonana naye
ili tusije tukawa kama wanawali waano wapumbavu ambao hawakujiweka tayari
(AMOSI 4:12; MATHAYO 25:1-13). Watu hawa
walimlaki kwa kutwa matawi ya mitende.
Matawi ya mitende, ilikuwa ishara ya ushindi mkubwa. Wakapiga kelele wakisema HOSANA! Hosana, ni neno la lugha ya KIARAMU, lenye
maana, “BWANA OKOA“. Wakapiga kelele,
wakimkiri yesu hadharani kwamba ni Mfalme wa Israeli na Masihi aliyetabiriwa
kwamba atakuja akiwa amepanda punda, naam mwana punda (ZEKARIA 9:9). Watu hawa waliotoka nje ya Yerusalemu
waliwazidi wakaao Yerusalemu na kumpokea Yesu kipekee. Wa kwanza, atakuwa wa mwisho, tusipoangalia
kwa makini! Sisi tunaojiona kwamba
tumekuja Kanisani muda mrefu na ni wenyeji, tuna hatari ya kupitwa na wale
wapya wanaokuja ikiwa tumekwisha kulizoea Neno kama watu wa Yerusalemu. Tunajifunza pia hapa kwamba, huduma zetu
huanzia chini, kwenye hori ya kulia ng’ombe, kama Yesu, lakini tukiwa waaminifu
na kuitenda kazi ya Mungu bila kujali upinzani tutakaoupata, hatimaye Bwana
atatupandisha juu sana, na watu watazishangilia huduma zetu.
(2)
UWEZEKANO WA WANAFUNZI WA YESU KUSHINDWA KUYAFAHAMU MAMBO FULANI
MWANZONI (MST. 16)
“Mambo hayo, wanafunzi wake hawakuyafahamu HAPO
KWANZA“. Inahitaji kufunuliwa na kutiwa
nuru macho ya miyo yetu, ili tuyaelewe mambo ya Mungu, yanapokuwa katika hatua
za mwanzoni (WAEFESO 1:17-18). Huduma ya
Paulo Mtume, ingawa ilitoka kwa Mungu mwenyewe, haikukubalika Yerusalemu,
walipokuwapo Mitume wenye karama mbalimbali (MATENDO 9:15,26; WARUMI 15:30-31). Hatupaswi kuona ajabu, wanafunzi wa Yesu
wanapokuwa hawafahamu kwamba huduma zetu zimetoka kwa Mungu. Ni kawaida katika hatua za mwanzo kwa
wanafunzi kutokuelewa mambo fulani fulani, lakini tukidumu kutenda kazi,
hatimaye yale yaliyofichika huwa wazi.
Tunaweza pia kujifunza somo fulani mwanzoni, tukawa hatulielewi; baadaye
ndipo ufahamu ukatujia. Ndiyo maana ni
muhimu sana kuomba kwamba Mungu atupe roho ya hekima na ya ufunuo katika
kulijua Neno lake na pia atutie nuru macho ya mioyo yetu ili tuyafahamu maneno yake
pale tu tunapoyasikia.
(3) SABABU YA MKUTANO MKUBWA KUMLAKI YESU
(MST. 17-18)
Mkutano mkubwa walikwenda kumlaki Yesu, kwa kuwa walisikia
kwamba alikuwa amefanya ishara ya kumfufua Lazaro kutoka kaburini. ISHARA, ni tendo lolote linalodhihirisha
waziwazi uwezo wa Mungu unaoweza kuyafanya yale yale yasiyowezekana kwa
wanadamu. Yesu Kristo alikuwa ametoa
mahubiri mazuri sana katika hekalu na masinagogi mengi Yerusalemu. Hata hivyo, hakuwahi kupata kuona mkutano
mkubwa hivi ukimlaki mpaka pale walipoona ishara hii kubwa. Hii inatufundisha umuhimu wa miujiza katika
injili ikiwa tunataka kuwavuta wengi kwa Yesu.
Neno peke yake, halitoshi, lisipoambatana na ishara (WARUMI
15:18-19). Hatuna budi kuomba ishara
kubwa zifanyike kati yetu kulithibitisha Neno, ili mkutano mkubwa uvutwe
(MATENDO 4:29-30; MARKO 16:19-20).
(4)
KUSHINDWA KWA SHETANI KUZUIA MAFANIKIO YA INJILI (MST. 19)
Pamoja na mabaraza ya Mafarisayo na maamuzi yao kinyume na
Yesu, bado umati mkubwa unamfuata hapa kiasi ya kwamba wanajiona hawafai neno
lolote maana ulimwengu wote unakwenda nyuma yake. Hatupaswi kubabaishwa na vita vya Shetani
katika huduma zetu. Kadri
anavyounguruma, ndivyo tunavyozidi kushinda na zaidi ya kushinda (WARUMI
8:35-37).
(5)
UTARATIBU WA KUMWONA YESU (MST. 20-23)
Mahali hapa kulikuwa kuna umati mkubwa waliotaka kumwona
Yesu, baada ya kusikia juu ya ishara aliyoifanya ya kumfufua Lazaro. Hata hivyo, kila mmoja hakuweza kumwona Yesu
tu kama alivyotaka. Kulikuwa na
utaratibu wa kufuata. Hapa tunaona
wakimwendea filipo na Filipo akaenda akamwambia Andrea kisha ndipo taarifa
zikamfikia Yesu na kuwa tayari kuwaona.
Katika Kanisa kubwa kama hili, hatuna budi kufuata utaratibu huu
pia. Kabla ya kumwona Mchungaji,
inatubidi tuwaone Viongozi wa makanisa ya Nyumbani, Seksheni, Zoni, Mhudumu
Mkuu n.k. Utaratibu huu ni wa lazima
kwenye umati mkubwa wa watu. Matatizo
yote yakimwndea mtu mmoja, siyo mapenzi ya Mungu, maana mengine yaliyo madogo
yanaweza kupata ufumbuzi kwa viongozi wengine (KUTOKA 18:13-26), na kumpa Kiongozi
wetu nafasi ya kutosha ya kuutafuta uso wa Mungu, na kushughulikia yale yaliyo
magumu.
(6) JINSI
YA KUTOA MAZAO MENGI (MST. 24)
Mbegu kabla ya kutoa mazao mengi, hufa kwanza, na kuzikwa
ardhini, ndipo huota na kutoa mazao mengi.
Yesu alikufa na kuzikwa, kisha akafufuka na kutuvuta wote kwake (MST.
32). Hatuwezi kupata mazao mengi, ikiwa
hatuko tayari kuona fedha zetu zainakufa pale tunapotoa fungu la kumi la mapato
yetu na sadaka. Hatuwezi kutoa mazao
mengi ikiwa tunajiona tunajua. Hatuna
budi kuzika kiburi na majivuno na lolote linalotufanya tujione tunajua; ndipo
tunapoweza kutoa mazao mengi.
(7) HATARI
YA KUIPENDA NAFSI (MST. 25)
Kuipenda nafsi yetu, ni kutaka kutimiza matakwa yote ya
miili yetu. Ni muhimu kufahamu kwamba
mwili, sikuzote hushindana na Roho zetu (WAGALATIA 5:16-17). Mwili hutaka tufanye yasiyo mapenzi ya
Mungu. Mwili hautaki tufanye maombi,
tusome Neno la Mungu, tushuhudie na kufuatilia watoto wachanga kiroho
n.ki. Mwili, hutaka tuupambe kinyume na
Neno la Mungu. Tukizipenda nafsi zetu,
hatuwezi kumtolea Mungu, kumtumikia au kufanya lolote linalompeneza Mungu. Matokeo yake, tutaziangamiza nafsi zetu. Hatuna budi kuzichukia nafsi zetu na kutiisha
miili yetu na kuzifanya roho zetu ziwe na utawala juu ya miili yetu na
kukatalia matakwa yake.
(8)
MASHARTI NA FAIDA ZA KUMTUMIKIA MUNGU (MST. 26)
Wengi wetu wanapenda kumtumikia Mungu, lakini hawajui masharti
ya kumtumikia. Sharti kubwa ni KUMFUATA
kwanza katika tabia (1 PETRO 1:15-16).
Tukijaribu kumtumikia bila kumfuata, tunalitukanisha Jina la Mungu wetu
bure (WARUMI 2:21-24). Tukiwa na tabia
ya Kristo, kisha tukamtumikia, pale alipo yesu, ndipo tutakapokuwa. Mungu Baba hutuheshimu na kutupa kipaumbele
katika mengine yote hapa duniani (KUTOKA 23:25-26; ISAYA 65:13-14). Hatimaye tutapata thawabu kubwa mbinguni kama
wafanyakazi bora wanavyopata tuzo katika Serikali na Mashirika. Tuzo ya Mungu ni ya kipekee mno.
(9) JINSI
YA KULIONA JINA LA BWANA LIKITUKUZWA KWETU (MST. 27-28)
Roho yake Yesu ilifadhaika kwa ajili ya dhambi zetu. Hili lilimfanya Baba alitukuze Jina lake
kwek. Sisi nasi, roho zetu zikifadhaika
kwa ajili ya dhambi za watu wengine na kuwaombea kwa kuugua ili waokoke, Jina
la Bwana litatukuzwa kwetu na tutaona mambo makubwa kama Habakuki (HABAKUKI
1:2-4).
…………………………………………………………………………………………………………………………………..
Ni sifa ipi ya kutuwezesha kuingia mbinguni? Ni utakatifu (WAEBRANIA 12:14). Ndani yake hakitaingia kamwe chochote kilicho
kinyonge (UFUNUO WA YOHANA 21:27).
Kinyonge ni kipi? Ni yule
anayetenda dhambi. Huyu ni mtu asiyefaa,
ni mnyonge! Je, wewe ni mtakatifu? Jibu ni la!
Maisha yako yamejaa dhambi, pamoja na kusema una dini; hivyo wewe pia ni
mnyonge, hufai kuingia mbinguni. Ukitubu leo dhambi zako zote kwa kumaanisha
kuziacha, na kuifuata njia ya Yesu Kristo, ndipo utakapopata rehema ya kuingia
mbinguni (MITHALI 28:13; YOHANA
14:6). Je, uko tayari kutubu sasa ili
upate rehema hii? Najua uko tayari. Basi fuatisha sala hii ya toba kwa dhati
kutoka moyoni; “Mungu Baba asante kwa
ujumbe huu. Hakika mimi ni mnyonge,
mwenye dhambi. Sistahili kuingia
mbinguni. Natubu dhambi zangu zote kwa kumaanisha kuziacha. Kuanzia leo nataka niifuate njia ya Yesu
Kristo. Bwana Yesu niwezeshe. Asante kwa kunisikia katika Jina la
Yesu. Amen”. Mpendwa msomaji umekubaliwa kuingia
mbinguni. Ili uzidi kudumu katika
utakatifu mpaka siku ya kuiaga dunia hii, hakikisha unahudhuria mafundisho
katika Kanisa linalohubiri wokovu. MUNGU
AKUBARIKI !!!
No comments:
Post a Comment