Jehanum ya Moto ni wapi na Kukoje?
ASKOFU ZAKARIA KAKOBE anasema
Miaka ipatayo thelathini iliyopita nilikuwa nimezama sana
katika dhambi. Nikiwa katika lindi hilo
la dhambi, sikutaka kusikia chochote kwa mtu yeyote aliyenieleza kwamba niache
dhambi, na eti niokoke. Niliwaona watu
wanaohubiri mambo ya kuokoka, wameshindwa maisha (frustrated),
wamechanganyikiwa na tena hawajasoma.
Nakumbuka siku moja, mhubiri mmoja alinihubiria na kuniambia, ”Acha
dhambi, au sivyo utatupwa katika Jehanum moto”. Unajua nilimjibuje! Nilimwambia, ”Wewe usinibabaishe na hiyo
Jehanum ya moto. Potelea mbali nikienda
motoni, pilipili usizozila zakuwashiani?
Usinifuate katika maisha yangu, chukua “time” yako!”
Baada ya miaka kadha kupita,nilipokuja kusikia mafundisho
kuhusu jinsi kulivyo huko Jehanum ya moto, nilikuja kufahamu kwamba yule
mhubiri nilimjibu potelea mbali nikienda motoni, kwa sababu tu sikuwa ninaelewa
lolote kuhusu jinsi Jehanum kulivyo; kwa kuwa sikuwahi kufundishwa mafundisho
hayo na kiongozi wangu wa dini. Tangu
niliposikia mafundisho hayo, maisha yangu yalibadilika kabisa. Mpendwa msomaji,
huenda hata wewe hujasikia mafundisho halisi kuhusu jinsi kulivyo Jehanum ya
moto, kama mimi nilivyokuwa; ndiyo maana nimeona leo nikushirikishe mafundisho
haya kupitia katika “note” hii. Mungu
akubariki kwa kuendelea kusoma “note” hii.
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . .
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . .
Potelea mbali nikienda motoni,
pilipili Usizozila zakuwashiani
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . .
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . .
Biblia
inaeleza waziwazi kwamba mtu anapokufa, sekunde ileile ya kufa kwake
anakabiliwa na hukumu. Tunasoma katika
WAEBRANIA 9:27, ”Na kama vile watu wanavyowekewa kufa mara moja, na baada ya
kufa hukumu”. Watu wanapofundisha
kinyume na kweli ya Neno la Mungu, hufundisha kwamba mtu anapokufa analala tu,
na hakuna lolote la hukumu mara moja wakitumia maandiko yafuatayo na
kuyatafsiri visivyo – MATHAYO 27:52; 1
WAKORINTHO 15:20; YOHANA 11:11-14 n.k;
na pia wanasema wafu hawajui lolote kwa kutumia maandiko kama MHUBIRI 9:5. Ilivyo ni kwamba, kinachobaki kaburini ni
mwili tu. Roho ya mtu huondoka na
kuingia katika mwili mwingine, unaoitwa mwili wa roho. Miili tuliyo nayo wanadamu kabla ya kufa
inaitwa miili ya asili. Tunasoma katika
1 WAKORINTHO 15:40, 44, “Tena kuna miili ya mbinguni, na miili ya
duniani,……Ikiwa uko mwili wa asili, na wa roho pia uko”.
Mwili wa asili, ndiyo unabaki kaburini, lakini roho ya mtu
huondoka kama tunavyosoma katika MHUBIRI 12:7, “Nayo mavumbi ya nchi kuirudia
nchi kama yalivyokuwa, nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa”. Mwili wa asili, ndiyo unaobaki kaburini, na
huo ndiyo unaotajwa kwamba umelala, haujui lolote, na hauna kumbukumbu; lakini
pasipo mwili huo, mtu atamwona Mungu na kukabiliana na hukumu yake dakika
ileile baada ya kufa (AYUBU 19:26).
Ikiwa mtu ameishi katika mapenzi ya Mungu, mara tu baada ya kufa
huchukuliwa mbinguni (LUKA 23:43; LUKA
16:22). Ikiwa ameishi na kufa katika
dhambi, bila kutubu dhambi zake na kuokoka, hukumu yake mtu huyo, huwa ni
kutupwa katika Jehanum ya moto, mara tu baada ya kufa, kama Yule tajiri
anayetajwa katika Biblia (LUKA 16:19-24).
Advertisements
REPORT THIS AD
Mbinguni ni juu (mbingu ya tatu), lakini kuzimu au Jehanum
ya moto, ni pande za chini za nchi (2 WAKORINTHO 12:1-4; MITHALI 15:24; ZABURI 63:9;
EZEKIELI 31:14). Mara mtu
anapokufa, hufika kwenye njia panda.
Kila mmoja hupenda kwenda mbinguni kuzuri, hata hivyo ikiwa jina lake
haliko katika kitabu cha uzima cha mbinguni, hulazimika kwenda Jehanum ya
moto. Mtu anayetakiwa kwenda motoni,
huchachamaa na kukataa kwenda kwenye njia mbaya inayotisha ya motoni. Hali hii wakati mwingine inaweza kuonekana
katika mwili wa asili kwa kumwangalia mtu anavyotapatapa na kuhangaika sana
katika kufa kwake. Kutokana na mtu
asivyopenda kwenda motoni na kutaka kwenda mbinguni asikotakiwa, mtu hulazimika
kukamatwa kwa nguvu na malaika wa kutisha, na kutupwa katika Jehanum ya moto;
inayojulikana pia kwa jina jingine, giza la nje; kama tutakavyoona baadaye
kidogo (UFUNUO 19:20; UFUNUO 20:10; MATHAYO 25:30).
Huko motoni Jehanum kukoje?
Mwanangu, kunatisha, nashindwa hata nikueleze vipi unielewe. Moto wa milele, hatukuwekewa wanadamu bali shetani
na malaika zake (MATHAYO 25:41). Kama
utakwenda huko baada ya kusoma “note” hii, itakuwa ni kwa sababu ya kiburi
chako tu, na kushupaza shingo yako na kukataa kulitendea kazi Neno hili
(MITHALI 29:1). Moto wa Jehanum siyo
mahali pa mchezo kama walimu wa uongo wanavyofundisha. Walimu hawa huwafariji watu na kusema eti mtu
ataunguzwa na moto na kutoweshwa na kupotea na kuangamizwa kabisa na ndiyo mwisho wake. Wanatumia maandiko
kama MATHAYO 10:28 (kuangamizwa) na
YOHANA 3:16 (Kupotea). Kuangamia katika
maandiko hakumaanishi kumalizika kabisa, bali kukabiliwa na mauti (ESTA
4:16). Mauti ya watu walioko motoni, ni
mauti ya milele, kama tutakavyoona hivi punde.
Kondoo akipotea, haimaanishi hayupo kabisa ila ametengwa na mchungaji
(ISAYA 57:1-3).
Vilevile, neno “kuharibu” linapotumika kuhusiana na adhabu
ya milele, halina maana ya kufanya kitu kisiwepo, bali ni kuadhibu vikali (1
WAKORINTHO 3:16-17). Walimu hawa wa
uongo, pia hufundisha kwamba, eti watu
watatoweshwa kama moshi baada ya kuunguzwa kwa kutumia andiko la ZABURI
37:20. Kutoweshwa hapa ni kutenganishwa
na Mungu, kama Adamu na Hawa walivyotoweshwa na kutolewa katika bustani ya
Edeni, na hivyo kutengwa na Mungu. Kwa
ujumla, mafundisho yote haya yanatokana na shetani, yanalenga kuwafanya watu
waendelee kutenda dhambi, huku wakipuuza ukweli juu ya Jehanum, kwa kuwaza
kwamba watateseka dakika chache na kupotea kabisa na ndiyo mwisho. Huu siyo
ukweli. Ukweli kuhusu Jehanum ya moto ni
upi basi? Sikiliza nikuambie!
Ukweli kuhusu Jehanum ya moto, ni upi basi? Jehanum ya moto, au kuzimu, ni shimo kubwa na
refu sana lililojaa moto. Wengi
tunafahamu jinsi wanawake wanavyouchochea moto wa kuni au mkaa, kwa kuupulizia
hewa kwa mdomo, au kipepeo. Sasa basi, moto wa Jehanum nao huchochewa
mfululizo, ili usizimike; lakini huchochewa na pumzi ya Bwana, yaani pumzi
maalum ya Mungu mwenyewe (ISAYA 14:15;
ISAYA 30;33). Moto wa Jehanum ni
mkali sana kuliko moto wowote tunaoufahamu duniani. Moto wa gesi wa kuunganishia vyuma,
unaotokana na kuwashwa mchanganyiko wa gesi ya “Oxygen”, na “Acetylene”,
unaonekana kwa hapa duniani kwamba ni mkali.
Moto huu, siyo chochote, ukilinganishwa na moto wa Jehanum. Katika karakana au viwanda vya vifaa vya
vyuma, chuma huyeyushwa na kuwa uji katika matanuru ya moto mkali unaofikia
nyuzi joto 2,000 hadi 3,000 na zaidi.
Moto huu unaoyeyusha vyuma na ukali wake, huo si chochote! (Kumbuka
kwamba maji yaliyochemka sana hufikia nyuzi joto 100 tu!) Moto ulio katikati ya jua linalotuangaza,
unafikia nyuzi joto milioni kumi (10,000,000°C). Moto wa jua nao, si chochote ukilinganishwa
na moto wa Jehanum! Ukali wa moto wa
Jehanum, unatisha (WAEBRANIA 10:26-27).
Siyo hilo tu, moto wa duniani una rangi mbalimbali, njano,bluu,mwekundu
n.k. Moto wa Jehanum ni tofauti kabisa;
Ni moto wa rangi nyeusi, unaosababisha giza na kumfanya mtu aliye motoni,
awaone wenzake wachache tu wa karibu naye, hivyo hamna faraja ya kusema “tuko
wengi!” Moto huu mweusi, ndiyo maana
unaitwa “giza la nje” (MATHAYO 8:11-12,
MATHAYO 22:13; MATHAYO 25:30; YUDA 1:6).
Siyo hilo tu. Moto huu wa
Jehanum, una meno! Hivyo una uwezo wa
kuwala na kuwatafuna walioko motoni (KUMBUKUMBU 32: 22; WAEBRANIA 10: 26-27). Hata hivyo, pamoja na moto huu kumtafuna mtu,
bado una sifa ya kumhifadhi mtu huyo na kumfanya asimalizike, kama jinsi chumvi
ilivyo na uwezo wa kuizua nyama kuharibika.
Hivyo moto unamtafuna mtu wakati wote, lakini haishi na wala moto
wenyewe hauzimiki. Ndiyo maana unaitwa
moto wa milele (MARKO 9: 43-49; MATHAYO
25:41).
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . .
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . .
Moto wa Jehanum, ni moto wa rangi nyeusi
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . .
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . .
Moto
huu wa Jehanum, huambatana na madini yanayoitwa kiberiti au kwa lugha ya
kitaaluma, “sulphur.” Kwa wale
wanaofahamu kidogo somo la shule la “kemia” au “chemistry,” wanafahamu kwamba
madini ya “sulphur”, yakiwashwa moto, huwa kama mpira, na hutoa harufu mbaya
kama ya mayai yaliyooza. Harufu ya namna
hii inafunika kuzimu yote, na watu walioko huko wanahangaika kushika pua zao,
lakini hakuna jinsi!. Hebu jaribu kuwaza
maisha haya, ndiyo yawe ya milele, mpendwa msomaji! Siyo hilo tu! Katika moto
huu, wamo funza maalum ambao huwatafuna watu na kufanya matundu mengi makubwa
katika miili yao, wakiingia na kutoka, kutoka ubavu hadi ubavu mwingine kutoka
kwenye tumbo hadi mgongoni n.k. Hii
hufanya sura za wale walioko motoni, kuwa mbaya mno kama madude tu! (ISAYA 14:
11; MARKO 9:43-49; ISAYA 66:24).
Hata kama mtu alikuwa mweupe duniani, huko motoni, huwa ni mweusi tii!
Moto wa milele, huitwa pia mauti ya pili (UFUNUO 21:8). Kwa nini huitwa mauti ya pili? Uchungu wa
mauti unaomfanya mtu kugugumia kwa mateso makali, akishindwa kupumua vizuri na
kubaki kusema “Mmh! Mmh! Mmh!”, mpaka watu wanasema heri afe apumzike, uchungu
wa jinsi hiyo humkabili mtu aliye motoni, milele na milele. Kwa lugha rahisi, ni kusema kwamba watu
walioko motoni, wakati wote wako katika hali ya kufa, lakini hawafi! Niseme nini mwanangu ili unielewe! Watu walioko motoni, hujawa wakati wote na
vilio, na tena husaga meno yao kama mtu anayeona baridi kali (MATHAYO 8:
12). Walioko motoni wanajifahamu, na
kuwakumbuka wenzao waliowaacha duniani, na tena wakati mwingi hutoa ndini zao
nje, kama mbwa, wakitamani maji kidogo kupoza ulimi kutokana na joto kali
linalosababisha kiu kubwa, lakini hawapati maji hata tone! Juu ya yote hayo katika vilio vyao, humwomba
Mungu awahurumie na kuwasamehe lakini Yeye amekwishasema, “Nami jicho langu
halitaachilia, wala sitaona huruma” (EZEKIELI 9: 10; EZEKIELI 8:18).
Watu walioko motoni, hutamani mtu mmoja kati yao atoke
motoni aje duniani, awashuhudie ndugu zao, ili waache dhambi, na kukwepa mateso
yao, lakini huambiwa kwamba ndugu zao wanapaswa kuyasikia maneno ya manabii
walioko duniani, maana hata akitumwa mtu kutoka motoni na kueleza mateso ya
huko, watasema ni mwongo, hajaenda motoni.
Tunasoma haya katika LUKA 16:27-31, ”Akasema, Basi, baba, nakuomba,
umtume nyumbani kwa baba yangu, kwa kuwa ninao ndugu watano, ili awashuhudie,wasije
wao pia wakafika mahali hapa pa mateso. Ibrahimu akasema, wanao Musa na
manabii, wawasikilize wao. Akasema, La, baba Ibrahimu, lakini kama akiwaendea
mtu atokaye kwa wafu, watatubu. Akamwambia, Wasipowasikia Musa na manabii,
hawatashawishwa (hawatashawishika) hata mtu akifufuka katika wafu”.
Mpendwa
msomaji, ikiwa mama yako mzazi alifariki akiwa hajaokoka, ujue yuko motoni, na
anakuambia, “Usinifuate huku mwanangu”.
Ikiwa baba yako mzazi alifariki akiwa dhambini, anateseka motoni, na
hataki umfuate huko aliko! Ndugu, marafiki
na jamaa zako walioko huko wanakukumbuka sana, na hawapendi ujiunge nao huko,
bali wanataka utubu na kuokoka mateso hayo ya moto. Walioko huko motoni, wakimwona yeyote
mwingine kutoka duniani, ambaye alikuwa na nafasi ya kusikia habari kama hizi
na akazipuuza, kisha akawafuata huko motoni, humwambia, “Je wewe nawe umekuwa
dhaifu kama sisi! Wewe nawe umekuwa kama sisi! ” (ISAYA 14: 10).
Mpendwa msomaji, baada ya kusikia yote haya kutoka kwa nabii
aliyetumwa kukuletea ujumbe huu, usifanye moyo wako kuwa mgumu. Hii ni nafasi ya kipekee ya kuokoka. Je, unajuaje kama utaamka kitandani baada ya
kulala usiku wa leo? Wakati uliokubalika
wa wokovu ni sasa (2 WAKORINTHO 6:2).
Labda utaniuliza, ili uokoke, ufanyeje?
Jibu ni rahisi, kwa imani ukitubu dhambi zako kwa kumaanisha kuziacha,
na kumwambia Yesu Kristo akusamehe, utasamehewa sasa hivi, na msamaha wa
dhambi, huambatana na wokovu (LUKA 1:77).
Je, uko tayari kuokoka sasa hivi?
Najua uko tayari. Basi fuatisha sala hii kwa dhati toka moyoni, “Mungu
baba asante kwa kuniletea ujumbe huu.Natubu dhambi zangu zote, kwa kumaanisha
kuziacha. Yesu Kristo nakuomba unisamehe dhambi zangu na kunipa uwezo wa
kushinda dhambi na kuniokoa kutoka katika mateso ya moto wa milele. Asante, kwa
kuniokoa katika Jina la Yesu.
Amen”. Tayari sasa umeokoka, na
kwa hakika unakwenda mbinguni sasa, hata ukifa leo. Ili uzidi kuukulia wokovu, hakikisha
unahudhuria mafundisho katika Kanisa linalohubiri wokovu. MUNGU AKUBARIKI !!!
No comments:
Post a Comment