FURAHA YA MUNGU KWA
WATENDAKAZI
Tunajifunza somo la msingi katika mfululizo wa masomo ya
Shule ya Uinjilisti, kwa kuligawa katika
vipengele vinne:-
( 1 ). KAZI TULIYOPEWA WATU TULIOOKOLEWA
( 2 ). UINJILISTI NI NINI?
( 3 ). NANI ANAHUSIKA NA UINJILISTI?
( 4 ). FURAHA YA MUNGU KWA WATENDAKAZI
( 1 ). KAZI TULIOPEWA WATU TULIOOKOLEWA
Siku chache kabla ya
Yesu Kristo kupaa mbinguni, alitukabidhi kazi ya muhimu sana ya kufanya. Kazi
hiyo, ni kuenenda ulimwenguni mwote na kuhubiri Injili kwa kila kiumbe, na
kuwafanya mataifa au watu wasiookolewa, kuwa wanafunzi wa Yesu, na kuwafundisha
kuyashika yote tuliyoamuriwa, baada ya wanafunzi hao kubatizwa kwa jina la Baba
na Mwana na Roho Mtakatifu. Akasema kwamba, tukishiriki kufanya kazi hii,
atakuwa pamoja nasi siku zote, hata ukamilifu wa dahari hata wakati atakaporudi
tena ( MARKO 16:15; MATHAYO 28:19-20 ). Hili ni Agizo Kuu la Yesu Kristo kwetu.
Wengi wetu tuliookolewa, hatumwoni Yesu Kristo akiwa pamoja nasi siku zote, kwa
sababu hatushiriki kikamilifu kuifanya kazi aliyotupa Yesu katika Agizo Kuu
hili. Kufanya kazi hii, ni kufanya kazi ya Uinjilisti.. Hili sasa, linatuleta
katika kipengele cha pili cha somo letu.
( 2 ). UINJILISTI NI NINI?
Uinjilisti ni
uvuvi wa watu ( MATHAYO 4:19 ). Kwa kuzaliwa na kutenda, watu wote ni wenye
dhambi na hivyo, wamekwisha kuhukumiwa na kutupwa katika ziwa la moto.
Uinjilisti, sasa, ni kuwapelekea watu hawa habari njema yaani Injili, kwa
kuwahubiria kwamba, yeyote kati yao atakayemwamini Yesu, atasamehewa hukumu
aliyokwisha kupata ya moto wa milele.
Tukifanikiwa kuwafanya watu hawa watoke
katika ziwa hilo la moto, kwa kufanya hivyo tumewavua kutoka ziwani, kama
kuwavua samaki ( YOHANA 3:18, 36; UFUNUO 21:8; YUDA 1:22-23 ). Hata
hivyo,Uinjilisti hauishii hapo. Kama vile mvuvi wa samaki asivyowaacha samaki wake aliowavua kwenye ufuo wa bahari au ziwa,
mahali ambapo wataoza, basi huwachukua mara moja na kuwahifadhi vizuri; au kama
mvuvi huyo wa samaki, asivyowaacha samaki
wake kwenye ufuo wa ziwa na wakatembea hapo, mwisho wakarudi ziwani,
vivyo hivyo, Uinjilisti au uvuvi wa watu, unakamilika kwa kuhakikisha wale
waliokata shauri kumwamini Yesu na kuokolewa, wanaendelea Kanisani au nyumbani
mwa Bwana, mahali ambapo watajifunza mafundisho ya mitume na kuukulia wokovu (
LUKA 14:23; YOHANA 15:16; MATENDO 2:41-42; 28:30-31; WAGALATIA 4:9-11, 19-20 ).
( 3 ). NANI ANAHUSIKA NA UINJILISTI?
Watu wengine,
kwa kukosa mafundisho, wanafikiri kwamba kazi ya uinjilisti, inafanywa tu na
Wainjilisti, Wachungaji, Walimu au Mitume na Manabii waliowekwa na Mungu maalum
kwa kazi hiyo na kupewa karama mbalimbali. Hii ni mbinu ya Shetani ya kufanya
kazi hii ifanyike kwa viwango vya chini, ili yeye afurahi kuona wengi
wanaangamia. Wainjilisti, Wachungaji, Walimu, au Mitumne na Manabii; ni
Makomanda au viongozi wa Jeshi, na watu wengine waliookoka ni askari wa jeshi
hili la Kristo Yesu ( 2 TIMOTHEO 2:3 ). Je, ni jeshi gani la nchi yoyote
linaloweza kushinda ikiwa watakaopigana ni makomanda wa jeshi hilo tu na askari
wengine hawashiriki kupigana? Jeshi la namna hiyo, ni lazima litashindwa
vibaya. Askari wa kawaida, ndiyo wengi sana na katika nchi yetu, Tanzania,
wanaitwa wapiganaji, maana bila wao, makomanda hawawezi kufanya kazi hiyo
wenyewe. Kazi ya makomanda ni kuwa mstari wa mbele wa mapigano, na
kuwaongoza maaskari wengine kuleta
ushindi.Hivi ndivyo walivyofanya Kanisa la kwanza. Uinjilisti, haukuachwa kwa
Mitume tu, pamoja na karama walizokuwa nazo; bali wote, wanaume na wanawake
katika Kanisa la kwanza walishiriki katika kufanya Uinjilisti ( MATENDO 2:17-18
).. Hata pale ambapo mitume walibaki Yerusalemu, wengine wote katika Kanisa,
walitawanyika nakwenda kulihubiri Neno. Ndiyo maana, Kanisa la Kwanza,
liliupindua ulimwengu wa nyakati zao ( MATENDO 8:1, 4 ). Mafundisho mengine ya
Biblia, pia yanaoana na jambo hili. Kila mtu aliyeokoka, amefanywa kuwa mfalme
na kuhani ( UFUNUO 5:9-10; UFUNUO 1:5-6 ).Utukufu wa Mfalme ni wingi wa watu
wake, na uchache wa watu wake ni uharibifu wake ( MITHALI 14:28 ). Mtu
ambaye hana hata mtu mmoja katika milki
yake, hawezi kudai kwamba ni mfalme. Mfalme wa nani? Mfalme wa hewa? Vivyo
hivyo, mtu aliyeokoka ambaye hana mtu yeyote katika milki yake aliyempata kwa
uinjilisti, huyu ni mfalme wa hewa. Kazi ya Kuhani pia, ni kumpatanisha mtu
aliyetenda dhambi, na Mungu wake, kwa kumfanya mtu yule kupata msamaha wa
dhambi kutoka kwa Mungu (MAMBO YA WALAWI 6:1-2, 6-7 ). Kwa misingi hiyohiyo,
kila mtu aliyeokoka, kwa kufanywa Kuhani; amepewa na Yesu Kristo, huduma ya
upatanisho, kuwapatanisha wenye dhambi pamoja na Mungu wao ( 2 WAKORINTHO
5:17-18 ). Kama Kristo alivyotumwa na Baba, anatutuma sisi pia kufanya huduma
ya upatanisho. Tusipofanya uinjilisti kwa wenye dhambi, tunawafungia katika
dhambi. Tukiwa wavuvi wa watu, tunafanya watu hao waondolewe dhambi, maana
watamwitaje Yesu bila kumsikia mtu akiwahubiri?
( YOHANA 20:21, 23; WARUMI 10:13-14 ). Tukiwafungia watu katika dhambi kwa
kuacha kufanya uinjilisti, tunamuwekea Mungu moshi machoni pake na kumfanya
atoe machozi, na vile vile tunampa siki anywe na kumfanya apate ganzi kwenye
meno. Siyo vema kwetu kumfanyia hivyo
Mungu ikiwa kweli tumeokolewa ( MITHALI 10:26 )
( 4 ). FURAHA YA MUNGU KWA WATENDAKAZI
Hakuna
lolote tunaloweza kulifanya kwa Mungu na kumfurahisha, kama kuwa watenda
kazi wanaofanya Uinjilisti, kwa kuwaleta watu kwa Yesu, na kuwalea katika
uchanga wao kiroho, mpaka waukulie wokovu. Kila mtu aliyeokoka, angependa na
kufurahi kuwa Mtendakazi, kama angejua ni kwa kiasi gani Mungu katika Utatu
(Baba, Mwana na Roho Mtakatifu) anavyomfurahia mtendakazi mmoja anayefanya kazi
ya uinjilisti. Ili tufahamu furaha ya Mungu kwa watendakazi ni muhimu tujifunze
Mungu ni nani kwetu tuliookoka, na sisi ni akina kwake:-
1. Mungu Baba ni Mkulima (YOHANA
15:1)-Mkulima anapopita kwenye shamba liwe la migomba, mikahawa, michungwa,
mipapai, minazi n., hufurahia sana kuona tawi linalozaa na kulishughulikia
sana. Tawi lisilozaa, huliondoa na kulitupa motoni (YOHANA 15:2). Mkulima akiona tawi la migomba
lililozaa mkungu na ndizi nzuri, atalitembelea tawi hilo wakati wote, na kuweka
mti ili kulikinga tawi hilo na upepo n.k. Ndivyo alivyo Mungu kwa mtendakazi wake.
2. Mungu ni Bwana wa Majeshi (YAKOBO
5:4)-Amiri Jeshi Mkuu, huwafurahia mno askari wapiganaji hodari ambao
wanaufanya ufalme wake kukua na kulindwa. Hawa humpa nguvu na sifa, hivyo
huwatunuku medali maalum za kitaifa. Ndivyo alivyo Mungu kwa watendakazi wake.
3. Mungu ni mwenye mali – Mungu anafananishwa na mtu mwenye mali
aliyesafiri ambaye amewaachia watumwa wake mali ili waifanyie biashara na
kupata faida. Mtu mwenye mali wa namna hii akirudi, atamfurahia sana mtumwa
yule aliyepeta faida kuliko yule aliyeificha tu, na hakuzalisha chochote
(MATHAYO 25:14-30). Ndivyo alivyo Mungu kwa mtendakazi wake.
4. Yesu ni Mfanyabiashara mwenye vyombo vya
uvuvi– Mfanyabiashara mwenye vyombo vingi vya uvuvi, huajiri wavuvi na kuwapa
vyombo vya uvuvi. Wanaporudi kutoka katika uvuvi, humfurahia sana yule
aliyeleta samaki wengi na kumpenda mno. Asiyeleta samaki, ana hatari ya
kunyang’anywa chombo na asipewe tena. Ndivyo alivyo Yesu kwa mtendakazi wake aliye mvuvi wa watu (MATHAYO 4:19).
5. Yesu ni Mfugaji mwenye zizi la Kondoo
–Baada ya kupotea Kondoo wengi katika zizi lake, anawatuma watu kuwatafuta.
Atamfurahia mtendakazi atakayerudi na Kondoo wake wengi waliopotea (LIKA
15:3-7)
6. Mungu ni mume wetu (YEREMIA 3;14)–
Mume humfurahia sana mke anayezaa sana
na kuwalea vizuri wanae. Asipozaa, upendo kati yao huingia dosari, na ndoa
huingia mashakani ikiwa ni mataifa. Ndivyo alivyo Mungu kwa mtendakazi wake.
7. Yesu ni Mpanzi wa Mbegu (MARKO 4:3)-
Hakuna linalomfurahisha Mpanzi kama mbegu ile iliyotoa mazao mengi. Baada tu ya
kupanda, mpanzi huanza kuangalia mbegu itakayoota na kutoa mazao mengi. Hiyo
huipenda mno. Ndivyo alivyo Yesu kwa mtendakazi wake.
8. Yesu ni Mwalimu (YOHANA 13:13)- Mwalimu
humfurahia sana mwanafunzi wake anayefanya kama yeye mwenyewe kutokana na jinsi
alivyomfundisha. Ikiwa mwalimu anamfundisha mtu udereva lakini mtu yule ni mzito wa kufanya kama mwalimu
wake, hapendezi kwake. Mtendakazi anayefanya Uinjilisti kama mwalimu wake Yesu,
anamfurahisha mno.
9. Roho Mtakatifu ni Bwana wa mavuno –
Anamfurahia sana mtu yule anayevuna roho za watu na kuzileta ghalani mwake,
kuliko yule anayeacha mavuno yaozee shambani (MATHAYO 9:38; MATENDO 13:2; YOHANA 4:35-36).
10. Mungu ni Baba kwetu (MATHAYO 6:8-9) –Baba
yeyote, hufurahi sana kuona watoto wa mtoto wake. Mungu pia hufurahi kuona
watoto wa mtendakazi. Kwa sababu Mungu anamfurahia mtendakazi:-
( a ). Uwezo wa majibu ya maombi yake huongezeka (YOHANA
15:16)
( b ). Atang’aa kama nyota milel (DANIELI 12:3).
( c ). Watoto wa mtendakazi humuongezea Ushindi juu ya
Shetani (ZABURI 127:4-5)
( d ). Watoto hao watakuwa ni taji ya kujionea fahari, furaha
na utukufu wake wakati wa kuja kwa Yesu (1 WATHESALONIKE 2:19-20)
No comments:
Post a Comment