AMRI MPYA
Leo, tena, Bwana ametupa neema ya kuendelea kujifunza Kitabu
cha YOHANA, katika Biblia zetu. Leo,
tutatafakari YOHANA 13:33-38, na YOHANA 14:1-3.
Katika mistari hii, pamoja na mambo mengine, tutajifunza kuhusu “AMRI
MPYA“. Tutayagawa mafundisho
tunayoyapata katika mistari hii katika vipengele tisa:-
(1) ENYI WATOTO
WADOGO (MST. 33);
(2) BADO KITAMBO
KIDOGO NIPO PAMOJA NANYI (MST. 33);
(3) MIMI NIENDAKO
NINYI HAMWEZI KUJA (MST. 33, 36-37);
(4) AMRI MPYA (MST.
34-35);
(5) KUUTOA UHAI KWA
AJILI YA YESU (MST. 37-38);
(6) MSIFADHAIKE
MIOYONI MWENU (MST. 1);
(7) MAKAO MENGI
MBINGUNI (MST. 2);
(8) NAKWENDA
KUWAANDALIA MAHALI (MST. 2);
(9) NITAKUJA TENA
NIWAKARIBISHE (MST. 3).
(1)
ENYI WATOTO WADOGO (MST. 33)
Hapa Yesu, alikuwa amekaa na mitume hawa, akiwafundisha kwa
zaidi ya miaka mitatu. Alikuwa amewapa
amri juu ya pepo wachafu, wawatoe na kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila
aina, na kufufua watu (MATHAYO 10:1,8).
Pamoja na yote haya, Yesu bado anaawaita “WATOTO WADOGO“. Ni muhimu kwa kila mmoja wetu, kujifunza
jambo la muhimu hapa. Hata kama sisi ni
Mitume, Manabii, Wainjilisti, Wachungaji, Waalimu, Viongozi wa Zoni, Seksheni
au Makanisa ya Nyumbani, hata kama tumepewa mafunuo au karama za namna ipi na
tunatumiwa jinsi gani na ungu, ni muhimu kufahamu kwamba Yesu, bado anatuita
“WATOTO WADOGO“. Ni watoto wadogo kwa
msingi kwamba hatujajua lolote bado, kama itupasavyo kujua (1 WAKORINTHO 8:2);
na tena pasipo Yesu Kristo, sisi hatuwezi kufanya neno lolote (YOHANA
15:5). Bdo wakati wote tunahitaji msaada
kutoka kwake Yesu. Hatuna haja ya kuwa
na kiburi wakati wowote ule. Kadri
tunavyokumbuka wakati wote kwamba sisi ni “Watoto wadogo“, na kumtegemea Mungu
katika kushinda kwetu, na kufanya lolote lile, ndivyo tunavyojiweka katika
nafasi nzuri zaidi ya kutumiwa sana na Mungu.
(2)
BADO KITAMBO KIDOGO NIPO PAMOJA NANYI (MST. 33)
Yesu hapa, anawaambia wanafunzi wake kwamba, bado kitambo au
muda mchache, ataondoka na kufa na kuzikwa; kisha kufufuka na kupaa
mbinguni. Anawaonya watumie vizuri muda
waliobaki nao kwa kumwuliza maswai, kuhusiana na yale aliyowafundisha, au siyo,
watamtafuta wasimwone. Kuna jambo la
kujifunza hapa. Kila mmoja wetu hana
budi kufahamu kwamba bado kitambo kidogo sana Yeye ajaye atakuja, wala
hatakawia (WAEBRANIA 10:37). Hivyo ni
juu ya kila mmoja wetu, kuukomboa wakati, na kufanya mapenzi ya Bwana (WAEFESO
5:15-17); na siyo, atakuja kulinyakua Kanisa na kutukuta hatujajiandaa. Leo yuko pamoja nasi akitufundisha na
kutuonya kila siku. Hatuna budi
kuyazingatia maonyo yake na kuyafuata wakati bado neema hii haijaondoka kwetu.
(3)
MIMI NIENDAKO NINYI HAMWEZI KUJA (MST. 3, 36-37)
Katika YOHANA 7:33-34; Yesu aliwaambvia Wayahudi kwamba
hawawezi kwenda pale anapokwenda (mbinguni) kwa sababu walikuwa hawakubali
kwamba Yeye ni Masihi na kuokoka. Sasa
hapa tena, anawaambia wanafunzi wake.
Kwa wanafunzi wake, anamaanisha kwamba, hawawezi kumfuata atakapokuwa
anakwenda kuteswa na kisha kusulibishwa.
Ndivyo ilivyokuwa, wanafunzi wote walimwacha na kukimbia (MATHAYO
26:56). Hata hivyo, Yesu alimwambia
Petro kwamba atamfuata baadaye, akimaanisha kwamba yeye naye baadaye atasulibishwa
(YOHANA 2:17-19). Ndivyo ilivyokuwa
kulingana na historia ya Kanisa la Kwanza, Petro naye alisulibishwa. Hata hivyo, alikataa kusulibishwa kichwa juu
miguu chini kama Bwana wake Yesu, akasulibishwa miguu juu kichwa chini.
(4) AMRI MPYA (MST. 34-35)
Yesu hapa, anatoa amri mpya kwa wanafunzi wake akisema,
“Mpendane, kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo“. Mtu yeyote aliyeokoka, anatazamiwa
kuitekeleza ami hii kwa kuwapenda wenzake waliokoka kama Yesu naye
alivyoonyesha upendo huo. Upendo kwa
watu wenzake waliokoka, ndiyo alama kuu inayomtambulisha mtu kwamba
ameokoka. Kwa alama hii, mtu aliyeokoka,
ATAJIJUA MWENYEWE kwamba ameokoka (1 YOHANA 3:14). Kwa alama hii pia, WATU WOTE WATAJUA kwamba
sisi tumeokoka (YOHANA 13:35). Vivyo
hivyo, kwa alama hii, MUNGU HUWAJUA watoto wake ( 1 YOHANA 3:10). Hatuwezi kudai kwamba tunampenda Mungu
tusiyemowna, ikiwa hatuawezi kuwapenda ndugu zetu waliookoka ( 1 YOHANA
4:20). Kumwamini Yesu au kuokolewa,
wakati wote huambaana na kuwapenda watu
waliokokaka (1 YOHANA 3:25; 4:21).
Yeyote yule anayedai kwamba ameokoka, lakini anawachukia ndugu zake
waliookoka, huyu ni mwuaji kwa msingi uleule ambao Kaini alivyokuwa wa yule
mwovu, akamwua ndugu yake Habili (1 YOHANA 3:11-12, 15). Imetupasa kupendana sisi kwa sisi kama Yesu
alivyotupenda sisi kwa kuzingatia yafuatayo:- (a) Yesu alijishughulisha na
ugonjwa wa mkwewe Petro, mwanafunzi wake (MARKO 1:30-31). Sisi nasi kama kweli tumeokoka hatuna budi
kuangaliana katika magonjwa na matatizo.
(b) Yesu alijishughulisha na msiba wa wanafunzi wake Martha na Mariamu
na kufadhaika pamoja nao juu ya kifo cha Lazaro (YOHANA 11:33-36), sisi nasi
upendo wetu kwa wengine unapaswa kudhihirika katika misiba (c) Yesu aliwatembelea wanafunzi wake majumbani
kwao (MARKO 1:29). Sisi nasi ikiwa kweli
tumeokoka, imetupasa kutembeleana majumbani kwetu (d) Yesu alihusika kumsaidia mwanafunzi Petro
alipokuwa ana tatizo la kifedha wakati yeye alikuwa ana uwezo wa kumsaidia
(MATHAYO 17:27). Sisi nasi inatupasa
kusaidiana katika matatizo ya kifedha, ikiwa kweli tumeokoka. Mtu akiwa na riziki ya dunia inampasa
kumwangalia ndugu yake aliyeokoka asiyekuwa na riziki (1 YOHANA 3:17-19). (e)
Yesu aliutoa uhai wake kwa ajili yetu, sisi nasi imetupasa kuutoa uhai
wetu kwa ajili ya wenzetu waliookoka, katika kuwahudumia wanpokosa nauli hata
kama sisi nasi tumebakiwa na kidogo tu, na kuwapa huduma nyingine kwa msingi
huu (1 YOHANA 3:16). (f) Yesu aliwapenda na kuwajali wanafunzi wake
kuliko wazazi na ndugu zake wa kimwili (MATHAYO 12:46-50). Sisi nasi hatuna budi kuwapenda watu wenzetu
waliookoka katika mambo yote, KULIKO ndugu zetu wa kimwili. Ikiwa mtu anadai ameokoka, na hana upendo wa
jinsi hii, madai yake si ya kweli.
(5) KUUTOA UHAI KWA AJILI YA YESU (MST. 37-38)
Watu tuliookoka, hatuna budi kuwa waaminifu katika imani ya
Yesu hata ibidi kufa, kama alivyowaza Petro hapa. Siyo tu kupigwa na kuwekwa gereani, bali tuwe
tayari hata kufa katika kuishindania imani (UFUNUO 2:10). Hatupaswi kuyahesabu maisha yetu kuwa kitu
cha thamani kuliko wokovu wetu (MATENDO 20:24).
Mitume walipigwa na kuaibishwa lakini hawakuahca wokovu (MATENDO
5:40-42; 16:19-23). Hata hivyo,
tusijivunie akili au kutumainia nafsi zetu katika kutenda haya, bali tumtumaini
Mungu mwenye kutupa neema ya kutuwezesha; ili tusije kuwa kama Petro
aliyejigamba kisha akamkana Yesu mara tatu.
(6)
MSIFADHAIKE MIOYONI MWENU (MST. 1)
Wanafunzi wa Yesu waliposikia Yesu akisema anawaacha kitambo
kidogo, walifadhaika mioyoni mwao.
Akawaambia, “Msifadhaike mioyoni mwenu, mnamwamini Mungu, niaminini na
mimi“. Hatupaswi kufadhaika mioyoni
mwetu wala kuwa na woga, bali tumtegemee na kumwamini Yesu kwamba ana uwezo wa
kutushindia katika magumu yoyote yanayotukabili (YOHANA 14:27).
(7)
MAKAO MENGI MBINGUNI (MST. 2)
Neno la Kiyunani linalotafsiriwa hapa “Makao“, ni
“MONE“. Neno linalotumika katika Biblia
ya Kiingereza ya KJV, “MANSIONS“, lina maana inayoleta picha halisi ya Neno
“MONE“, kuliko neno la Kiswahili “MAKAO“, “MANSION“, ni jumba kubwa la
kifahari. Jumba la Meya wa Jiji la
London, Uingereza (Lord Mayor of London), linaitwa “MANSION HOUSE“. Kila mtu aliyeokoka, ameandaliwa jumba kubwa
la kifahari sana huko mbinguni. Mpaka
sasa majumba haya au makao haya, bado mengi sana yakitungojea kuyaingia. Yesu anatuhakikishia jambo hili. Jumba lako linakungoja, Je, utaliingia?
(8)
NAKWENDA KUWAANDALIA MAHALI (MST. 2)
Yesu amekwenda kutuandalia mahali kama mtu anayeandaa
vyakula mezani. Hatimaye atakuja
kutukaribisha wote tule na kunywa mezani pake (LUKA 22:29-30).
(9)
NITAKUJA TENA NIWAKARIBISHENI (MST. 3)
Yesu atakuja kutukaribisha mezani wakati wa Kunyakuliwa kwa
Kanisa (1 WATHESALONIKE 4:16-17). Baada
tu ya kunyakuliwa, tutafanyiwa Karamu katika Harusi ya Mwanakondoo. Tujiweke tayari maana hatuijui siku wala saa
(LUKA 12:37,40).
…………………………………………………………………………………………………………………………………..
Ni sifa ipi ya kutuwezesha kuingia mbinguni? Ni utakatifu (WAEBRANIA 12:14). Ndani yake hakitaingia kamwe chochote kilicho
kinyonge (UFUNUO WA YOHANA 21:27).
Kinyonge ni kipi? Ni yule
anayetenda dhambi. Huyu ni mtu asiyefaa,
ni mnyonge! Je, wewe ni mtakatifu? Jibu ni la!
Maisha yako yamejaa dhambi, pamoja na kusema una dini; hivyo wewe pia ni
mnyonge, hufai kuingia mbinguni. Ukitubu leo dhambi zako zote kwa kumaanisha
kuziacha, na kuifuata njia ya Yesu Kristo, ndipo utakapopata rehema ya kuingia
mbinguni (MITHALI 28:13; YOHANA
14:6). Je, uko tayari kutubu sasa ili
upate rehema hii? Najua uko tayari. Basi fuatisha sala hii ya toba kwa dhati
kutoka moyoni; “Mungu Baba asante kwa
ujumbe huu. Hakika mimi ni mnyonge, mwenye
dhambi. Sistahili kuingia mbinguni.
Natubu dhambi zangu zote kwa kumaanisha kuziacha. Kuanzia leo nataka niifuate njia ya Yesu
Kristo. Bwana Yesu niwezeshe. Asante kwa kunisikia katika Jina la
Yesu. Amen”. Mpendwa msomaji umekubaliwa kuingia mbinguni. Ili uzidi kudumu katika utakatifu mpaka siku
ya kuiaga dunia hii, hakikisha unahudhuria mafundisho katika Kanisa
linalohubiri wokovu. MUNGU AKUBARIKI !!!
( Full Gospel)
No comments:
Post a Comment