Ina maana gani kwamba mshahara wa dhambi ni mauti?

Warumi 6:23 inasema, "Kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti; bali karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu." Katika msingi wake, dhambi ni uasi dhidi ya Mungu. Dhambi zetu hututenganisha na Mungu, Muumba na mwenye uzima. Yesu alisema, "Mimi ndimi njia na kweli na uzima" (Yohana 14: 6). Mungu anajulikana kama "MIMI NDIMI" mkuu. Uzima uu katika Mungu. Kwa hivyo, tunapofanya dhambi na kujitenganisha na Mungu, tunatengana na uzima wa kweli. Kwa hivyo, bila shaka, tunakumbana na mauti. Hoja tatu za ufafanuzi zinahitajika: Kwanza, dhambi hasa haisababishi kifo cha kimwili mara moja. Warumi 6 haituambii kwamba tunapofanya dhambi tutakufa kimwili. Badala yake, inarejelea kifo cha kiroho. Pili, wakati tunapookoka katika Kristo, tunaokolewa kutokana na hatima ya kifo cha kiroho na kuletwa katika hatima ya uzima wa kiroho. Paulo aliwaambia Warumi, "Zawadi ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu" (Warumi 6:23). Tatu, hata dhambi za waumini bila shaka zitasababisha aina ya "kifo" cha kiroho. Ingawa tumeokolewa kutokana na adhabu ya mwisho ya dhambi (kutengwa kwa milele na Mungu), hatuokolewa kutokana na matokeo ya asili ya uhusiano uliovunjika na Baba . Tunapofanya dhambi, tunapata dalili za kifo cha kiroho. Tunaweza kujihisi kuwa na hatia, kuwa wapungufu, kuchanganyikiwa, au kutokuwa na uhusiano na Mungu. Sisi hufanya kama waadilifu badala ya kuwa wenye haki. Dhambi zetu, hata kama waumini, huumiza moyo wa Mungu na uhuzunisha Roho Wake (Waefeso 4:30). Ingawa dhambi zetu haziachi uhusiano wetu na Yeye, huweka kizuizi kati yetu. Fikiria mtoto na mzazi. Wakati mtoto anapoasi, uhusiano na mzazi wake unafadhaika. Mzazi bado anampenda mtoto na bado ana nia bora kwa mtoto moyoni. Mtoto kamwe aachi kuwa bila mzazi. Hata hivyo, mtoto anaweza kupata matokeo fulani: kutoaminiwa, nidhamu, hisia ya hatia, na kadhalika. Bila shaka hatimaye uhusiano hurejeshwa ila kawaida pigo huja kwanza. Hivyo ni pamoja nasi na Mungu. Tunapoasi dhidi ya utawala wa Mungu katika maisha yetu, tunaasi dhidi ya Uzima, na hivyo tunakumbana na mauti (kuvunjika kunaosababisha maumivu). Tunapomrudia Mungu, tunarudishwa tena kwenye ushirika wa kiroho na Mungu, hisia za lengo, haki, uhuru, nk. Baba mwenye furaha katika mfano wa Mwana mpotevu alisema vizuri zaidi: "Huyu mtoto wangu alikuwa amekufa na yu hai tena "(Luka 15:24).

CHAKULA CHA YESU KRISTO

 

CHAKULA CHA YESU KRISTO

Leo tena, tunazidi kusonga mbele katika kujifunza Kitabu cha YOHANA katika Biblia zetu.  Leo, tunajifunza YOHANA 4:27-45.  Pamoja na mafundisho mengine tutakayojifunza katika mistari hii, tutajifunza pia juu ya “CHAKULA CHA YESU KRISTO“.  Tutayagawa mafundisho yote tunayoyapata katika mistari hii, katika vipengele vinane:-

 

(1)UHUSIANO WA WANAUME NA WANAWAKE KATIKA WOKOVU (Mst. 27);

 

(2)WAJIBU WA KUUACHA MTUNGI (Mst. 28-30);

 

(3)CHAKULA CHA YESU KRISTO (Mst. 31-35);

 

(4)MSHAHARA WA KUMTUMIKIA MUNGU (Mst. 37-38);

 

(5)MMOJA HUPANDA AKAVUNA MWINGINE (Mst. 37-38);

 

(6)NENO LA MWANAMKE (Mst. 39);

 

(7)WALIMSIHI AKAE KWAO (Mst. 40-42);

 

(8)NABII HAPATI HESHIMA KATIKA NCHI YAKE (Mst. 43-45).

 

 

 

(1)      UHUSIANO WA WANAUME NA WANAWAKE KATIKA WOKOVU (Mst. 27)

 

Yesu Kristo, aliangalia sana uhusiano wake na wanawake kwamba hauleti dosari yoyote katika usafi wake na ushuhuda wa wokovu wa Injili yake.  Alipokuwa akisema na mwanamke Msamaria pale kisimani, wanafunzi wake walistaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke.  Siyo kwamba Yesu alikuwa hasemi na wanawake kabisa, la hasha!  Alisema nao (LUKA 10:41; 23:28-31; 8:47-48; YOHANA 20:16-17).  Katika tukio la kisimani, wanafunzi wake walishangaa kumwona Yesu akiwa na mwanamke yule Msamaria peke yao.  Hawakuwahi kuona hivyo kabla.  Lakini hata hapa, utaona kwamba ilikuwa ni hadharani – kisimani, mahali ambapo watu wanaingia na kutoka na kuyasikia yote waziwazi.  Ndiyo maana “hakuna aliyesema, Mbona unasema naye?“  Wakati wote, katika lolote, Yesu Kristo alikuwa mwangalifu katika lolote alilolifanya na wanawake.  Aliangalia kwa makini na kuhakikisha kwamba hakuna yeyote atakayesema “Wokovu ni uongo au Injili anayohubiri siyo ya kweli“.  Mtume Paulo vivyo hivyo, alipokuwa anakwenda nyumbani kwa mwanamke Lidia, hakuwa peke yake, alikuwa na wenzake Timotheo na Sila.  Katika timu walifanya kazi miongoni mwa wanawake.  Maneno “Tukaenda“, “Tukaketi“, “Tukasema“, “Akatusihi“, “Ingieni“, yanaonyesha kwamba walikuwa wengi (MATENDO 15:40-41, 16:1-2, 13-15).  Katika utendaji wake wa kazi, pale Paulo Mtume alipokuwa peke yake, alimchukua Akila na Prisila mkewe, wakaenda kutenda kazi na kuwa huru kuingia katika nyumba yoyote au kusema na yeyote.  Mtume Paulo, hakwenda na mwanamke Prisila katika Injili bila kuwa na mumewe.  Sisi nasi hatuwezi kufanya hivyo.  Hakuna kielelezo chochote cha wokovu wetu tunaohubiri, ikiwa mwanaume atakuwa anatembea barabarani au kuzunguka huko na huko, na mwanamke ambaye siye mke wake, kwa kisingizio cha kuitenda kazi ya Bwana (MATENDO 18:1-4).  Baada ya kuokolewa, tunapaswa kuhakikisha SIKU ZOTE kwamba tunakuwa na dhamiri isiyo na hatia.  SIYO MBELE ZA MUNGU TU, ILA NA MBELE ZA WANADAMU, ili mtu asije akatulaumu kwa habari ya karama hii tunayoitumikia yaani WOKOVU (MATENDO 24:16; 2 WAKORINTHO 8:20-21).  Watu ambao hawajaokoka wakimwona mwanaume aliyeokoka anatembea barabarani huku na huko na mwanamke ambaye siye mke wake au wako chumbani peke yao kwa visingizio vya kujifunza Biblia na kuomba; watasema wanafanya uasherati, hata kama siyo kweli.  Tayari hiyo ni hatia.  Uasherati haupaswi kutajwa kwetu kamwe hata kwa kudhaniwa (WAEFESO 5:3).  Mataifa wakiona wokovu siyo kweli kutokana na uhusiano wetu na wanawake, tendo hilo ni kuwawekea vikwazo vya kuwazauia kuingia mbinguni, wakati sisi wenyewe hatuingii (MATHAYO 23:13; LUKA 11:52; ISAYA 57:14; WALAWI 19:14; 1 YOHANA 2:10).  Kutembeleana kwa “kaka“ na “dada“ katika wokovu kwa visingizio vya kutembeleana katika ugonjwa n.k; vinaweza kuleta zinaa katika wokovu (2 SAMWELI 13:6-15).  Mwanaume atamshika mwanamke asiye mke wake mkono tu, katika salamu; siyo mabega, nywele au sehemu yoyote nyingine.  Wanawake watawafuatilia wanawake na vivyo hivyo wanaume.  Hakuna “boyfriend“ au “girlfriend“ katika wokovu.  Hata wachumba ni mwiko kutembeleana na kupikiana vyumbani mpaka baada ya ndoa.  Hata kuja kanisani mwanaume hapaswi kuzungumza na mwanamke mambo yasiyopasa kwa mfano “Binti mbona nyinyi wanawake mnatukataa wanaume kila tunapowachagua muwe wake zetu?“  Huo ni uasherati.

 

(2)      WAJIBU WA KUUACHA MTUNGI (Mst. 28-30)

 

Tukitaka kumpendeza Mungu, ni lazima tuwe tayari kuiacha mitungi yetu na kwenda kufanya kazi ya Mungu.  Mtungi ni chochote kinachoonekana ni cha muhimu kwetu duniani.  Ni lazima tuache biashara zetu na kwenda Kanisani au kufuatilia watoto wachangas kiroho.  Lolote lile iwe watoto, mume, kazi ya Kaisari n.k; yote hayo ni mitungi.  Tusiruhusu yatuzuie kumtumika Mungu.  Mwanamke huyu alipoacha mtungi wake, aliwaleta wengi kwa Yesu.  Asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wa Yesu (LUKA 14:3).

 

(3)      CHAKULA CHA YESU KRISTO (Mst. 31-35)

 

Chakula kwa mwanadamu, ni kitu ambacho tunakitolea muda wetu wote.  Katika kufanya kazi tunatafuta chakula, tunatumia saa nyingi kwa siku katika kula asubuhi, mchana na usiku.  Bila chakula cha mchana, wengine wataona maisha magumu mno.  Chakula cha Yesu Kristo kilikuwa kuyatenda mapenzi ya Mungu yaani kuihubiri Injili ili watu waokoke kama kwa mwanamke huyu Msamaria.  Hicho ndicho kilichokuwa chakula Na. 1, kwa Yesu.  Chakula cha mwili kilifuata baadaye.  Sisi nasi inatupasa kumfuata kwa kutoa maisha yetu yote kuihubiri Injili na kuwasimamisha watoto wachanga katika wokovu (YOHANA 13:15; 1 PETRO 2:21).

 

 

 

(4)      MSHAHARA WA KUMTUMIKIA MUNGU (Mst. 36)

 

Mshahara mkubwa unamsubiri kila mtu anayetoa muda wake mrefu kumtumikia Mungu.  Wengi kwa kutokuelewa, wanafikiri kumtumikia Mungu ni kazi isiyo na faida.  Inaweza ikaonekana hivyo hapa duniani, lakini kama tungepata ufahamu, kila mmoja wetu angetafuta kwa bidii, kumtumikia Mungu, kwa gharama yoyote; ili ajilimbikizie mshahara tele wa milele mbinguni (ISAYA 49:4; 2 NYAKATI 15:7; 1 WAKORINTHO 15:58).

 

 

 

(5)      MMOJA HUPANDA AKAVUNA MWINGINE (Mst. 37-38)

 

Kabla ya wanafunzi wa Yesu, manabii wengi walikufa kwa ajili ya Neno la Mungu.  Yohana Mbatizaji pia alikatwa kichwa kwa ajili ya Injili na wengi wengine.  Yesu naye ilimpasa kufa kwa misingi hiyohiyo.  Hata baadaye mitume nao walikufa vivyo hivyo, pamoja na wamishonari wengi.    Wote hawa wamepanda, nasi tunavuna hivi leo.  Tunaweza kumhubiri mtu asiokoke.  Tumepanda mbegu kwa kufanya hivyo atakuja kuvuna mwingine.  Yote ni sawa, tuzidi kuitenda kazi (1 WAKORINTHO 3:6-8; MHUBIRI 11:4-6).

 

(6)      NENO LA MWANAMKE (Mst. 39)

 

Neno la Mwanamke Msamaria siku ileile aliyokuwa ameokoka, lilileta watu wengi kwa Yesu.  Wanawake hatupaswi kujidharau. Mungu huwatumia wanawake kipekee kuwaleta wengi kwa Yesu, pale tu wanapoondoa kujidharau na kujiamini.  Wako manabii wengi waliokuwa wanawake katika Biblia – Miriamu (KUTOKA 15:20), Hulda (2 WAFALME 22:14), Noadia (NEHEMIA 6:14), Debora (WAAMUZI 4:4), Anna (LUKA 2:36).  Shime tuitende kazi ay Bwana.  Siyo kwa uwezo wetu, bali kwa uwezo wa Mungu tunaitenda kazi (ZEKARIA 4:6; WARUMI 9:16).

 

(7)      WALIMSIHI AKAE KWAO (Mst. 40-42)

 

Walipomsihi Yesu akae kwao zaidi, uamsho uliendelea.  Sisi nasi inatupasa kuendelea kumsihi Yesu na Roho Mtakatifu kwa maombi kila siku, ili uamsho uendelee kati yetu, ikiwa wanakaa kwetu.

 

(8)      NABII HAPATI HESHIMA KATIKA NCHI YAKE (Mst. 43-45)

 

Yesu Kristo, hakupokelewa vema na kupata heshima, Nazareti, hapo alipolelewa (LUKA 4:16, 22-30; MATHAYO 13:54-55).  Sisi nasi itakuwa hivyo.  Tunaweza tukawashuhudia ndugu zetu wasikubali ushuhuda wetu.  Ikiwa hivyo, tuwaunganishe na wale wasiowajua.

 

…………………………………………………………………………………………………………………………………..

 

Ni sifa ipi ya kutuwezesha kuingia mbinguni?  Ni utakatifu (WAEBRANIA 12:14).  Ndani yake hakitaingia kamwe chochote kilicho kinyonge (UFUNUO WA YOHANA 21:27).  Kinyonge ni kipi?  Ni yule anayetenda dhambi.  Huyu ni mtu asiyefaa, ni mnyonge!  Je, wewe ni mtakatifu?  Jibu ni la!  Maisha yako yamejaa dhambi, pamoja na kusema una dini; hivyo wewe pia ni mnyonge, hufai kuingia mbinguni. Ukitubu leo dhambi zako zote kwa kumaanisha kuziacha, na kuifuata njia ya Yesu Kristo, ndipo utakapopata rehema ya kuingia mbinguni (MITHALI 28:13;  YOHANA 14:6).  Je, uko tayari kutubu sasa ili upate rehema hii?  Najua uko tayari.  Basi fuatisha sala hii ya toba kwa dhati kutoka moyoni;  “Mungu Baba asante kwa ujumbe huu.  Hakika mimi ni mnyonge, mwenye dhambi.  Sistahili kuingia mbinguni. Natubu dhambi zangu zote kwa kumaanisha kuziacha.  Kuanzia leo nataka niifuate njia ya Yesu Kristo.  Bwana Yesu niwezeshe.  Asante kwa kunisikia katika Jina la Yesu.  Amen”.  Mpendwa msomaji umekubaliwa kuingia mbinguni.  Ili uzidi kudumu katika utakatifu mpaka siku ya kuiaga dunia hii, hakikisha unahudhuria mafundisho katika Kanisa linalohubiri wokovu.  MUNGU AKUBARIKI !!! ( FULL GOSPEL)

 

No comments: